NA WILLIUM PAUL, SAME.
MKUU wa Wilaya ya Same Mkoani Kilimanjaro Kasilda Mgeni ameongoza Wananchi wa Kijiji cha Ruvu Mbuyuni Kata ya Mabilioni katika harambee ya kuchangia uibuaji ujenzi wa Zahanati ya kijiji hicho kuondoa adha wanayokabiliana nayo ya kulazimika kutembea umbali wa Kilomita 25 kutoka kijijini hapo hadi Kituo cha Afya Hedaru kilichopo Kata ya Hedaru kufuata huduma za Afya.
Wakizungumza kwenye Mkutano wa hadhara uliofanyika Kijijini hapo wa kusikiliza na kutatua kero na malalamiko ya Wananchi, baadhi yao wamesema zipo changamoto nyingine ambazo wanakabiliana nazo kwenye Kijiji chao ikiwemo kukosa miundombinu mizuri ya barabara, maji safi na umeme.
Lakini suala la kukosa Zahanati kwao limekuwa changamoto kubwa sana ambalo linahitaji ufumbuzi wa haraka kwani yapo matukio ya kuwapoteza wapendwa wao, lakini pia mama waja wazito kujifungua wakiwa njiani kuelekea Kituo cha Afya hedaru kupata msaada wa matibabu.
Aidha kufuatia kwa hali hiyo, Kasilda alilazimika kuongoza harambee hiyo na kufanikiwa kukusanya zaidi ya shilingi Milioni 4.3 pamoja na vifaa vya ujenzi ikiwa ni pamoja na Saruji, Mchanga, Mabati, na Maji.
“Kutoka Ruvu Mbuyuni hadi Hedaru kilometa 25 ni mbali sana, kwenye hili lazima tuwe kitu kimoja jamani wakati Serikali inaendelea na mpango wake mimi naomba kama eneo lipo tuanze msaragambo haraka (nguvu kazi) Serikali itakuja kumalizia" Alisema Kasilda.
29 сен 2024