Kwa Waingereza kuna ule usemi wanaita “Jack of All Trades”, ina maana kinara kwenye kila fani. Tofauti na waingereza walipomalizia na “master of none”…inatia moyo pale unapomkuta “Jack and Master of All Trades”. Hapa namzungumzia Bi. Maria Sarungi-Tsehai.
Hivi karibuni wengi mmemsikia na kumuona katika mitandao ya kijamii akiwa mmoja kati ya vinara wa mijadala mbalimbali ya kijamii na kimaendeleo akishiriki katika mada mbalimbali, na zaidi pale panapotumika kivumishi cha #ChangeTanzania kwenye mitandao ya Twitter na Facebook. Lakini kwa wale wanaofuatilia vyombo vya habari kwa muda, watakuwa wanamfahamu Maria vizuri akiwa kama muandaaji wa vipindi mbalimbali vya Burudani na Kielimu vya Televisheni, ambavyo vilipata nafasi ya kurushwa na runinga mbalimbali hapa nchini.
Kwa wale walio na Mrengo wa tansia ya Mitindo na Unyange, basi jina la Maria halikua geni masikioni mwao, kwani ni mmoja wa wadau mstari wa mbele kwenye masuala ya mitindo, naye akiwa mmoja kati wa wanamitindo (model) waliowahi kufanya kazi na wapiga picha mashuhuri nchini. La zaidi, ni mmoja wa waandaji waandamizi wa Shindano la Urembo na Fani la “Miss Universe”, na hadi sasa matunda ya kazi zake yameonekana kutokana na wanamitindo kadhaa waliopita kwenye kambi yake kuonekana kufanya vizuri sana ndani na nje ya nchi.
Kwa wengi wanaomfahamu Maria, hawakushangazwa na kasi yake ya kujihusisha na siasa na harakati za ukombozi wa fikra hapa nchini kutokana na kukulia katika familia yenye mseto wa Kiutamaduni. Baba yake mzazi pia ni mmoja wa wanasiasa waliowahi kuvuma sana nchini na mtaalamu wa tiba ya mifupa, Profesa Philemon Sarungi. Malezi ya wazazi wake yalimpa ujasiri ambao ulimshawishi Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mh. Jakaya Kikwete kumteua kuwa mmoja wa Wajumbe 201 kutoka taasisi mbali mbali za kijamii na kisiasa waliokuwa sehemu ya Bunge Maalumu la Katiba mapema mwaka huu. Tofauti za kiitikadi na msimamo wake thabiti kwenye kile alichokiamini, vilimfanya Maria kugomea kurudi Bungeni wakati wa awamu ya pili ya vikao hivyo, hali iliyopokelewa kwa mtazamo tofauti na wale waliomtegemea kuwawakilisha.
Wenye hekima wanasema, Mwana Mpe Elimu apate maarifa ya kufanya maamuzi. Mwana mpe uhuru wa kufikiri, apate ujasiri wa kukabili changamoto. Maria ni mfano hai wa hili, Mjasiriamali, Mwanamitindo, Mwanahabari, Mwanaharakati na Mhamasishaji….zaidi ya yote…rafiki wa wengi.
Msikie kwa ukamilifu hapa, alipohojiwa na Kikosi cha Mkasi TV
Follow MkasiTV on
Facebook : / mkasitv
Twitter : @MkasiTV
14 окт 2024