Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam (RC), Albert Chalamila ameagiza kuondolewa majina 891 ya wafanyabiashara yaliyowekwa kwenye mtandao wa Shirika la Masoko Kariakoo mpaka pale vyombo vya dola vitakapojiridhisha na majina hayo.
Hatua hiyo inakuja baada ya wafanyabiashara zaidi ya 800 waliokuwepo sokoni hapo kabla ya soko kuungua Julai 2021 kuandamana jana Alhamisi, Julai 11, 2024 kwenda Ofisi za CCM Lumumba kupinga kutorejeshwa.
Katika orodha hiyo, wafanyabiashara 891 kati ya 1,861 ndio walioelezwa kuwa na vigezo vya kurejea. Uamuzi huo uliwafanya kujitokeza katika viwanja vya Mnazi Moja kuhakikiwa na baada ya kutoridhishwa ndio wakaandamana.
Chalamila ametoa maagizo hayo leo Ijumaa Julai 12, 2024, alipozungima na uongozi wa Shirika la Masoko Kariakoo katika Ofisi ya Shirika la Masoko Magogoni.
11 июл 2024